![Manchester City Win Premier League Title](http://media.skynews.com/media/images/generated/2014/5/11/308208/default/v1/team-celebrate-use-this-1-778x437.jpg) |
Wachezaji wa City wakishangilia ubingwa. |
Mbio za ubingwa wa ligi kuu ya Uingereza zimemalizika rasmi leo huku kila timu ikivuna ilichokipanda. Haikua rahisi kama ilivyokuwa kwa Bayern Munich ambao walishinda kikombe cha ligi kuu ya Ujerumani (Bundesliga) huku wakiwa wamebakiza mechi kibao. Ligi hiyo ambayo ni namba moja kwa kupendwa kote Duniani na ambayo pia ina ushindani mkubwa imemalizika kwa Manchester City kunyakua kombe hilo kwa tofauti ya pointi 2 mbele ya Liverpool ambao walipigana kufa na kupona ili kurudisha heshima yao.Katika mchezo wao wa leo ambao walimenyana na Westham United, Man City walihitaji sare ya aina yoyote ile ili kuchukua ubingwa huo lakini walichomoza na ushindi wa mabao 2-0, mabao yakifungwa na Samiri Nasri na nahodha Vicent Company. Huu ni ubingwa wa 4 wa ligi kuu ya Uingereza toka klabu hii ianzishwe mwaka 1894 ikiwa imechukua ubingwa mwaka 1936-37, 1967-68, 2011-12 na 2013-14.
![Manchester City Win Premier League Title](http://media.skynews.com/media/images/generated/2014/5/11/308202/default/v1/pitch-invade-1-778x437.jpg) |
Mashabiki wa City wakishangilia Ubingwa katika uwanja wao wa Etihad
Wadau wengi wa soka wameonekana kuridhishwa na ubingwa huu kwenda kwa Man City huku wakidai kuwa timu hiyo imestahili ubingwa huo ukilinganisha na maandalizi yake kuanzia umiliki, aina ya wachezaji na kocha Manuel Pellegrin ambaye amepata mafanikio katika msimu wake wa kwanza akiwa na City. |
![Manchester City fans hold a banner about their team's manager Manuel Pellegrini.](http://media.skynews.com/media/images/generated/2014/5/11/308104/default/v2/488671157-1-778x437.jpg) |
Mashabiki wa City wakionesha mapenzi yao kwa kocha wao Pellegrin |
Mbali na kombe la ligi Man City pia wameshinda kombe la Capital One. Katika mbio hizo za ubingwa Liverpool ambao walikua wanapewa nafasi kubwa ya kuibuka mabingwa, wameishia nafasi ya pili huku Chelsea wakimaliza katika nafasi ya tatu huku Big Four ikifungwa na Arsenal. Liverpool wamerudi katika nafasi nne za juu kwa mara nyingine tangu mwaka 2009 huku mabingwa wa msimu uliopita 2012-13 Manchester United wamemaliza msimu nje ya nne bora kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1990.
Timu tatu ambazo zimeporomoka daraja ni Cardiff, Fulham na Norwich.